Monday, March 18, 2024

HJFMRI KUTOA MILIONI 500 KWAAJILI YA KUTEKELEZA MRADI WA DREAM, MBEYA NA SONGWE

Mkurugenzi Mkuu wa HJFMRI Tanzania Sally Chalamila akizungumza wakati wa hafla ya kukabidhiwa mashine za kisasa na vifaa mbalimbali kwa mabinti balehe na wasichana vijana kupitia mradi wa dreams Wilaya ya Kyela Mkoa wa Mbeya.
Mwakilishi wa balozi wa Marekani nchini na Mtaalam wa masuala ya kuzuia maambukizi ya UKIMWI kutoka , WRAIR-DOD Dkt. Elick Kayange akizungumza kuhusiana na mradi wa Dreams.

Shirika la kimataifa la HJFMRI limesema linatarajia kutoa Sh 500 milioni  kuwezesha mabinti balehe na wasichana vijana kupitia mradi wa dreams kwa ufadhiri wa Mfuko wa Dharura wa Rais wa Marekani wa kukabiliana na UKIMWI (PEPFAR)

Mkurugenzi Mkuu wa HJFMRI Tanzania, Sally Chalamila amesema hayo Machi 16 mwaka huu wilayani Kyela wakati wa hafla fupi ya kukabidhi vifaa mbalimbali na mashine za kisasa vyenye thamani ya Sh 178 milioni.

Mashine na vifaa hivyo vimetolewa na Shirika la HJFMRI kupitia WRAIR-DOD kwa ufadhiri wa Mfuko wa Dharura wa Rais wa Marekani (PEPFAR) kwa kushirikiana na Asasi ya Tumaini.

Amesema lengo ni kuisaidia serikali kukabiliana na afua mbalimbali za maambukizi ya VVU kwa kuwezesha kundi hilo ambalo liko katika hatari kubwa ya kupata maambukizi.

Amesema mradi wa dreams umeanza kutelekezwa mwaka 2016 huku ukiwafikia mabinti balehe na wasichana vijana 130,000 huku katika Mkoa wa Mbeya ukitekelezwa katika Halmashauri tatu za Mbeya Jiji, Mbarali na Kyela.

Amesema Shirika hilo linatekeleza afua za matunzo na matibabu ya VVU katika Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini kupitia mpango wa Dreams katika Mkoa wa Mbeya na Songwe.

“Shirika linatekeleza afua za VVU kwa ufadhiri wa Mpango wa Dharura wa Rais wa Marekani kupitia Taasisi ya WRAIR-DOD huku takwimu zikionyesha mabinti walio katika umri mdogo ni wahanga wakubwa sana wa maambukizi ya VVU".

Chalamila ametaja miongoni mwa sababu ni jitihada za kutaka kujikwamua kiuchumi wanajikuta wakijiingiza katika tabia hatarishi ambazo kusababisha kupata maambukizi ya VVU.

Kwa upande wake Mwakilishi wa Balozi wa Marekani nchini na  Mtaalam wa masuala ya kuzuia maambukizi kutoka, WRAIR-DOD, Dkt. Elick Kayange amesema matokeo ya mapambano dhidi ya UKIMWIyamelata matokeo makubwa.

Amesema kwa takwimu za mwaka 2016/17 na kurudiwa 2022/23 zimeonyesha ongezeko la watu walioanza dawa na kufubaza ni asilimia 55.7 mpaka 87.4 huku waliofubaza imeongezeka kutoka asilimia 51.1 mpaka 84.6 kwa Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini.

Amesema hayo ni matokeo makubwa sana licha ya kuhitaji hitihada zaidi ili kufikia 0 tatu na kusiwepo kwa maambukizi ya VVU na unyanyapaa kwa wagonjwa.

Akizungumza kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu, Jenister Mhagama, Mkuu wa Wilaya ya Rungwe, Jaffar Haniu ameshukuru Shirika la HJFMRI kwa kuwezesha upatikani wa vifaa kwani vitawezesha Vijana  kujikwamua kiuchumi.

Aidha ametaja miongoni mwa changamoto kwa mabinti kujiingiza kwenye maisha hatarishi na kupata maambukizi ni kutokana na ukosefu wa vyanzo stahimilivu vya kujiingizia kipato.

Kwa upande wake Mratibu wa Tume ya Kudhibiti Ukimwi (TACAIDS) Mikoa ya Mbeya na Songwe, Emmanuel Petro amesema kuwa mradi wa Dreams unatekelezwa katika halmashauri 89 kwa Mkoa wa Mbeya ni Mbarali, Mbeya Jiji na Kyela.

No comments:

Post a Comment