Wednesday, February 7, 2024

SUMA JKT YAPATA TENDA YA UZOAJI TAKA KATA TANO ZA JIJI LA MBEYA

Halmashauri ya Jiji la Mbeya imekabidhiwa magari 11 na Kampuni tanzu ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) Suma JKT kwa ajili ya kuanza mkataba wa  uondoshwaji wa taka katika kata tano.

Kampuni hiyo imepata  zabuni kati ya makampuni 16 yaliyojitokeza, huku ikieleza malengo yake ni  kuhakikisha Halmashauri ya Jiji la Mbeya inarejea katika nafasi ya kwanza kwa usafi katika Majiji kutoka nafasi ya mwisho.

Akizungumza na waandishi wa juzi baada ya kukabidhi magari hayo, Mkurugenzi mwendeshaji  kampuni ya usafi, Kepteni Rosemary Katani amesema wamejipanga kurejesha  hali ya usafi kwa Jiji la Mbeya.

“Tumejipanga kuhakikisha Jiji linarejea kwenye nafasi nzuri katika suala la usafi, kwa sasa tumekuja na vifaa vya kisasa na nguvu kazi kwa vijana 50 watakaofanya kazi usiku na mchana taka zote zinaondolewa kwa muda mfupi” amesema Nchimbi.

Ametaja  miongoni mwa kata walizoingia mkataba ni  Kata Ilomba, Iyela, Forest, Sisimba na Ruanda  na kwamba watashirikiana na uongozi wa chini wa Serikali kuhakikisha suala la usafi linapewa kipaumbele kutokana na taarifa za kukithiri kwa uchafu.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Mbeya, John Nchimbi amekiri  Jiji kushika nafasi ya mwisho katika majiji nchini kwa  uchafu ikiwepo kutozolewa taka kwa wakati  na kwamba kupitia mkataba na kampuni ya Suma JKT inakwenda kuwa suruhisho.

“Kwa sasa tumeanza kusaini  mkataba wa mwaka mmoja na Suma JKT kama watafanya  vizuri  tunaongeza muda wa miaka mitatu, lengo ni kuona suala la uchafu linakuwa mwisho  ili kurejea katika nafasi ya kwanza kutoka nafasi ya mwisho” amesema.

Nchimbi amesema kuwa kutokana na maandalizi mazuri ya kampuni hiyo ni matarajio yake  jamii itoe  ushirikiano wa kulipa ada za taka ambapo kwa kila kaya ni Sh 2,000 tofauti na mikoa mwingine nchini.

“Leo hii tumefikia hatua ya kuingia mkataba ni msukumo wa Mkuu wa Mkoa, Juma Homera, Mbunge wa Mbeya mjini, DkT. Tulia Ackson na Mkuu wa Wilaya kuhakikisha  tunapata  mzabuni kutokana na kukithiri kwa uchafu” amesema Nchimbi.

Mkazi wa Mabatini  Lucy Nyailosi ameomba Serikali kupitia  kampuni iliyopewa zabuni ya  kukusanya ada za taka kutumia mfumo mzuri sambamba na kuelimisha jamii .

“Uwekwe mfumo mzuri wa ukusanyaji wa ada za taka ili jamii iweze kulipa bila shuruti sambamba na ratiba maalumu ya uondoaji wa kata katika kata tano” amesema.


No comments:

Post a Comment