Thursday, February 29, 2024

MICHE YA MATUNDA NA KIVULI ZAIDI YA 100 YAPANDWA SHULE YA MPAKANI WILAYANI KYELA


Taasisi ya Living Together Youth Foundation (LTYF) imeendelea na kampeni ya kufungua klabu za mazingira shuleni sanjari na upandaji miti ya matunda na kivuli katika maeneo ya shule, taasisi za umma na binafsi lengo likiwa ni kuhifadhi mazingira pia kujipatia lishe kutokana na matunda pamoja na kujiongezea kipato na kupata vifaa vya ujenzi.

Akizindua klabu ya mazingira na kuendesha zoezi la upandaji miche zaidi ya mia shule ya mchepuo wa kiingereza ya Mpakani, Mkurugenzi wa LTYF Leonatha Likalango amesema watoto wakipewa elimu ya mazingira watakuwa mabalozi wazuri kwani elimu hiyo wataifikisha kwa wazazi wao nyumbani.

Shule hiyo ni mpya na haina miti ya matunda na vivuli hivyo miti hiyo itasaidia kuzuia mmomonyoko wa udongo, upepo, kuwapatia matunda watoto na kuifanya shule iwe na mandhali nzuri na ya kuvutia.

Likalango amelez kuwa changamoto ya taasisi hiyo changa ni ukosefu wa fedha kwa ajili ya kugharamia ununuzi wa mbegu za miti pamoja viriba kwa ajili ya uoteshaji miti ili zoezi hili liifikie nchi nzima kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Rais Dkt Samia Suluhu Hassan ambaye amekuwa mstari wa mbele kupambana na uharibifu wa mazingira.

Mwalimu Mkuu wa shule hiyo Vitalis Mlambia ameishukuru taasisi ya Living Together Youth Foundation kwa uzinduzi wa klabu shuleni hapo na kuendesha zoezi la upandaji miti.

"Naahidi kuisimamia vema miti iliyopandwa ili itunzwe vizuri na kila mtoto amepanda mti wake ambao atautunza kipindi chote atakachokuwa shuleni" alisema Mlambia.

Baadhi ya wanafunzi Esther Patrick, Neema Jackson, Patrica Frank, Sekela Panja na Meshack Makumbusho wamesema kila wakifika shule huhakikisha wanaiangalia miti yao na kuifanyia palizi na umwagiliaji mara kwa mara ili isikauke.

Meneja wa taasisi ya Living Together Youth Foundation Noel Kayombo amesema wajibu wake ni kubaini maeneo yenye changamoto ya mazingira ili kuhakikisha nchi nzima inafikiwa na elimu ya utunzaji wa mazingira kwa kuhakikisha jamii inapanda miti pia kuacha utupaji hovyo wa chupa za maji na vinywaji.

Hivi karibuni taasisi ya Living Together Youth Foundation (LTYF) yenye makao makuu wilayani Kyela itafanya zoezi la upandaji miti makao makuu ya Polisi Wilaya ya Kyela ukiwa ni mwendelezo wa kutunza mazingira na vyanzo vya maji.

No comments:

Post a Comment