Sunday, January 21, 2024

MASACHE AKABIDHI GARI LA WAGONJWA HOSPTALI YA WILAYA CHUNYA.


Mbunge wa Jimbo la Lupa Masache Kasaka amekabidhi gari la Wagonjwa kwa uongozi wa Hosptali ya Wilaya ya Chunya ambayo ilipandishwa hadhi kutoka kituo cha afya.

Masache amesema gari hilo la wagonjwa (Ambulance) limetolewa na Rais Samia Suluhu Hassan kwa ajili ya kuboresha huduma za afya katika vituo vya Kambikatoto na Lupa Wilayani humo.

Amesema Serikali itaendelea kuboresha sekta ya afya ambapo imetoa zaidi ya Sh 2.5 bilioni kwa ajili ya ujenzi wa majengo nane sambamba na Sh 400 milioni kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba.

“Kama inavyofahamika hosptali hii awali ilikuwa kituo cha afya, Serikali ikapandisha hadhi na kuwa Kituo cha Afya, miundombinu yake ilikuwa sio rafiki lakini kwa kipindi cha miaka miwili tunashuhudia miundombinu imeboreshwa  chini ya Serikali ya awamu ya sita” amesema Masache.

Masache pia amewataka wananchi kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali sambamba na kuwataka kushiriki kikamilifu katika uchaguzi mdogo wa Serikali za mitaa unaotarajia kufanyika hivi karibuni.

“Sitarajii kuona kuna watu wengine watachukua fomu kuwania nafasi hiyo kwani hawa waliopo wanatosha wameonyesha uwezo mkubwa kushiriki katika usimamizi wa miradi ya Maendeleo iliyoelekezwa na Serikali” amesema Masache.
Kwa upande wake Mganga mfawidhi wa hosptali hiyo, Dkt. Dorison Andrew amesema kitendo cha Serikali kutoa gari la wagonjwa (Ambulance) litasaidia kuondoa changamoto kwa wagonjwa wanaotoka Kata za Lupa na Kambikatoto .

"Tunatarajia huduma kuboreshwa zaidi na wagonjwa kupata huduma kwa wakati tofauti na hapo awali kilikuwa na changamoto ya magari ya wagonjwa", amesema Dkt. Andrew.

Mmoja wa wanawake, ameishukuru Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan kwani upatikanaji wa gari hilo utaokoa maisha ya wakinamama wajawazito wanaoishi maeneo ya pembezoni.

No comments:

Post a Comment