Umeme wageuza vijiji kuwa vituo vya maendeleo; shule, biashara na kilimo vyanufaika…
Na Sanula Athanas aliyekuwa Shinyanga
KIJIJI cha Masunula katika Kata ya Usule, Wilaya ya Shinyanga mkoani Shinyanga, kina historia inayofanana na mamia ya vijiji vingine nchini.
Kilianzishwa mwaka 1974 kupitia Operesheni Vijiji (1973-1976), mkakati wa Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Nyerere, uliolenga kuwakusanya wananchi katika maeneo maalum ili kurahisisha utoaji huduma za msingi kama elimu, afya, maji na miundombinu mingine ya maendeleo.
Kwa miongo mitano, wakazi wa Masunula waliishi maisha ya kawaida ya vijijini yaliyotawaliwa na matumizi ya mafuta ya taa kwa mwanga, mashine zinazotumia dizeli kwa shughuli za uzalishaji na uhaba wa huduma nyingi za kisasa zilizokuwa zikionekana kama haki ya wakazi wa mijini pekee.

