Wednesday, November 3, 2021

KESI YA MBOWE YAAHIRISHWA, SHAHIDI APATWA NA TATIZO LA KIAFYA

 

Shahidi wa sita katika kesi inayomkabili Mwenyekiti wa CHADEMA Freeman Mbowe alitarajiwa kuanza kutoa ushahidi leo Jumatano Novemba 3, 2021 katika Mahakama Mahakama Kuu Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi.

Wakili wa Serikali Mwandamizi Robert Kidando, ameiomba Mahakama iahirishe kesi mpaka kesho kwa kuwa shahidi wao amepata tatizo la kiafya.

“Shauri linakuja kwa ajili ya kusikilizwa. mpaka jana kuna shahidi ambaye tulikuwa tumepanga kuendelea naye lakini amepata tatizo la kiafya. Hivyo tunaomba ahirisho mpaka kesho tutakapoweza kuendelea. Suala hili liko nje ya uwezo wetu,” amesema Kidando.

Kwa Upande wa utetezi ukiongozwa na wakili Peter Kibatala wamekubaliana na ombi hilo, lakini wakitaka upande wa mashtaka kuhakikisha wanaleta shahidi.

“Kwa kufuata amri ya Mahakama ya jana sisi tulikuwa tumejiandaa lakini kwa kuwa mambo yako hivi hatuna namna ila tunaomba tu wenzetu wajitahidi kesho tarehe 4 tuweze kuendelea,” amesema Kibatala.

Jaji Joachim Tiganga ameahirisha kesi hiyo hadi Kesho Alhamisi Novemba 4, 2021.

“Kufuatia maombi ambayo yameletwa na wakili Serikali kwamba shahidi waliyekuwa wamemwandaa amefika mahali hawezi kuja kutoa ushahidi kwa sababu zilizoelezwa za kiafya na kwa kuzingatia kuwa upande wa utetezi haukupinga basi maombi haya yanakubaliwa na shauri hili linaahirishwa hadi kesho.

“Upande wa mashtaka mnakumbushwa kuanda mashahidi ili tuweze kuendelea. Washtakiwa mtaendelea kuwa chini ya uangalizi wa Magereza,” ameeleza Jaji Tiganga.

Mbowe anakabiliwa na mashtaka ya uhujumu uchumi na kupanga kutekeleza ugaidi. Washtakiwa wengine katika kesi hiyo ni Halfan Bwire Hassan (mshtakiwa wa kwanza), Adamu Hassan Kasekwa maarufu Adamoo na Mohamed Abdillahi Ling’wenya.

Monday, November 1, 2021

MAADHIMISHO YA WIKI YA MSAADA WA SHERIA 2021 KUFANYIKA KITAIFA MKOANI MBEYA

Mh. Juma Homera, Mkuu wa Mkoa wa Mbeya.

 Na Keneth Mwakandyali.

Wananchi mkoani wa Mbeya wametakiwa kujitokeza kwa wingi kutumia fursa ya Maadhimisho ya Wiki ya Msaada wa Sheria inayofanyika kitaifa mkoani hapa kuanzia Novemba 01 hadi Novemba 12 katika viwanja vya Ruanda Nzovwe.

Wito huo umetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Juma Homera leo Novemba alipokua akitoa akizungumza na waandishi wa Habari ambapo amewataka wananchi kuchangamkia fursa hii ili kuweza kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili.

“Kutakuwa na timu ya wataalamu watakaokua wanazunguka maeneo mbalimbali ya wazi, vizuizini, mashuleni kutoa elimu wa msaada wa kisheria katika Nyanja tofauti kama ardhi, ndoa, mirathi, haki za wanawake, watoto na watu wenye ulemavu kuanzia Novemba 01 mpaka Novemba 07”
 
“Kuna changamoto nyingi kwenye secta hii ndio maana shughuli hii ya wiki wa msaada wa kisheria kufanyika kitaifa mkoani Mbeya inakwenda kuleta fursa kwa wananchi wenye changamoto mbalimbali kuweza kujua haki zao” alisema Homera
 
Naye mratibu wa Chama cha Sheria Tanganyika Kanda ya Mbeya Gerinus Mzanila amewahimiza wananchi kujitokeza kwa wingi kupata fursa ya kuweza kusaidiwa changamoto za kisheria walizonazo na kujitanua katika nyanja za kisheria.
 
“huduma ya msaada wa kisheria ni huduma ambayo inatolewa kwa mtu ambae hana uwezo wa kumudu gharama za huduma ya kisheria, zile ambazo zinatolewa mahakamani au kwa wakili. Huduma ya kisheria ipo katika nyanja nyingi kama vile kumuhoji na kusikiliza jambo lake, kumsaidia kuandaa nyaraka anazotakiwa kwenda kuzisajili mahakamani, usuluhishi wa amani, pia kutoa elimu kuhusiana na mambo mbalimbali ya kisheria” amesema Mzanila 
 
Aidha Afisa Maendeleo ya Jamii  Mkoa wa Mbeya Stella Kategile ameeleza kuwa wiki ya msaada wa kisheria imekua msaada mkubwa katika jamii kwani imejikita zaidi katika kutoa msaada kwa wananchi ambao hawana kipato na kushindwa kumudu gharama za huduma ya kisheria.